Wednesday, June 20, 2012

Wednesday, June 20, 2012

Marehemu Willy Edward aagwa leo viwanja vya mnazi mmoja jijini Dar

 Baadhi ya Wahariri wa Vyombo mbali mbali vya Habari hapa nchini wakijiandaa kushusha jeneza lenye mwili wa Mhariri wa Gazeti la Jambo Leo,Marehemu Willy Edward Ogunde aliefariki dunia mwishoni mwa wiki mkoani Morogoro.Shughuli ya kuaga Mwili wa Marehemu Willy imefanyika leo katika viwanja vya Mnazi Mmoja Jijini Dar na baadae ikafuatia safari ya kwenda Nyumbani kwao Mara kwa Mazishi.
 Mchungaji akiongoza ibada ya Kuaga Mwili wa Marehemu Willy Edward leo.
 Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri nchini,Absalom Kibanda akisoma historia fupi ya Marehemu Willy Edward wakati wa Kuaga mwili wake leo kwenye Viwanja Vya Mnazi Mmoja jijini Dar.
 Katibu wa NEC,Itikadi na Uenezi (CCM),Nape Nnaupe akizungumza kwenye shughuli hiyo ya kuaga Mwili wa Marehemu Willy Edward.
 Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF),Prof. Ibrahim Lipumba akitoa neno kwa wafiwa wakari wa shughuli ya Kuaga mwili wa Marehe Willy Edward leo.
 Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP,Dkt. Reginald Mengi akimpa pole Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Jambo Concepts ambao ni Wachapishaji wa Magazeti ya Jambo Leo,Juma Pinto wakati wa Shughuli ya Kuaga mwili wa Marehemu Willy Edward ambaye alikuwa ni Mhariri wa Gazeti la Jambo leo,iliyofanyika leo kwenye Viwanja vya Mnazi Mmoja,Jijini Dar.
Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP,Dkt. Reginald Mengi akitoa heshima zake za mwisho kwa Mwili wa Marehemu Willy Edward ambaye alikuwa Mhariri wa Gazeti la Jambo Leo aliefariki ghafla huko mkoani Morogoro mwishoni mwa wiki.
Katibu wa NEC,Itikadi na Uenezi (CCM),Nape Nnaupe akitoa heshima zake.
Bw. Athuma Hamis akitoa heshima za mwisho kwa Mwili wa Marehemu Willy Edward.
Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF),Prof. Ibrahim Lipumba akitoa heshima zake za mwisho kwa Mwili wa Marehemu Willy Edward ambaye alikuwa Mhariri wa Gazeti la Jambo Leo aliefariki ghafla huko mkoani Morogoro mwishoni mwa wiki.Hafla hii ya kuaga imefanyika mchana huu katika viwanja vya Mnazi Mmoja,Jijini Dar.
Mwili wa Willy Edward ukiwekwa katika sehemu yake tayari ibada ya kuaga.
Waombolezaji wakitoa heshima zao za mwisho.
Ankal akiwa na Mwanalibeneke Francis Godwin
Ankal akisabahiana na Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF),Prof. Ibrahim Lipumba,Katibu wa NEC,Itikadi na Uenezi (CCM),Nape Nnaupe pamoja na Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP,Dkt. Reginald Mengi.
Ankal akiwa katika mazungumzo na Katibu wa NEC,Itikadi na Uenezi (CCM),Nape Nnaupe.
Baadhi ya Wahariri wa Vyombo Mbali mbali vya habari nchini wakiwa katika picha ya pamoja.
Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri nchini,Absalom Kibanda akibadirishana mawazo na Mkuu wa Masoko wa Benki ya NMB,Iman Kajura.
Mwili ukipakiwa kwenye gari tayari kwa safari ya Mara kwa Mazishi.
Waombolezaji.

Tuesday, June 19, 2012


Zitto Kabwe.
Kambi rasmi ya upinzani bungeni imewasilisha bajeti mbadala ya kambi hiyo kwa mwaka wa fedha 2012/2013 na kuitaka serikali kuwa makini katika kukopa nje ya nchi kutokana na kukua kwa kasi kwa deni la taifa na kupendekeza pia magari ya kifahari ya serikali yapigwe mnada ili kupunguza matumizi ya mafuta.
Pamoja na hizo ishu kambi hiyo imeitaka serikali kuainisha njia za kudhibiti mfumuko wa bei unaowaongezea mzigo wananchi na kuwaongezea mishahara walimu, madaktari na wauguzi kwa asilimia 50 huku ikiweka mpango wa kuanza kuwalipa pensheni wazee wenye umri wa zaidi ya miaka 60.
Mbunge wa Kigoma Kaskazini kwa ruhusa ya Chadema Zitto Kabwe ambae pia ni waziri kivuli wa fedha amesema “swala ni kwamba tunakopa ili kufanya nini? bajeti ya mwaka 2012/2013 inayopendekezwa inaonyesha kwamba serikali itakusanya trilioni 8.7 kama makusanyo ya ndani na itatumia shilingi trilioni 10.6 kama matumizi ya kawaida, ni dhahiri kwamba sehemu ya mikopo ambayo serikali inachukua sasa itakwenda kwenye matumizi ya kawaida, hatutaki mikopo kwa ajili ya matumizi ya posho”
Kabwe amekamilisha kauli yake akikaririwa akisema “tuchukue mikopo kuwekeza kwenye miradi itakayokuza uchumi na kuzalisha kodi zaidi, kuiacha serikali kuendelea kukopa bila mpango ni kuliweka taifa rehani, hatuwezi kukubali wazee wetu waishi maisha yao waishi maisha yetu na wakope maisha ya watoto wetu”
Wabunge mbalimbali walichangia bungeni Dodoma June 18 2012 na kulalamikia kuongezeka kwa deni la taifa, usimamizi mbaya wa rasilimali za nchi na ugumu wa maisha kwa mtanzania na wengine wakakataa kuiunga mkono bajeti hiyo.


.
Ikiwa ni wiki moja tu imepita toka kutokea ajali ya Helikopta huko Kenya iliyochukua maisha ya watu sita wakiwemo mawaziri wawili, asubuhi ya June 18 2012 wasiwasi ulienea tena  kwenye mji wa Karatina huko Kenya baada ya HELIKOPTA kutua ghafla shambani kutokana na hali mbaya ya hewa kwenye anga.
Standard Media wamesema mwandishi wao wa eneo la mlima Kenya amesema hiyo helikopta ni ya raia wa kigeni aitwae Allan Root  aliekua akiwapeleka watoto wake shule Nairobi.
Root anaishi kwenye eneo la Mbuga ya LEWA na alipofika eneo la Karatina alilazimika kutua kwa ghafla katika shamba moja eneo la Mathaithi karibu na Karatina kutokana na hiyo hali mbaya ya anga ambayo kama angeendelea kusafiri kulikua na uwezekano mkubwa wa ajali kutokea.


Laurent Blanc.
Stori kwenye kila mtaa unaofatilia soka la nje hazikosi jina la club ya Tottenham ambayo imempiga chini juzi kocha wake ambae ni Harry Redknapp na sasa inatafuta kichwa kipya kwa ajili ya hiyo nafasi.
Sky Sports wamesema club hiyo sasa hivi imeweka macho yake kwa kocha wa Ufaransa Laurent Blanc (46) ambae mkataba wake na Ufaransa unakwisha baada ya michuano ya Euro ambapo inaaminika anaweza kurudi kwenye Premier League.
Kwa sasa wako kwenye mazungumzona Laurent japo sio kocha peke yake ambae wanafanya nae mazungumzo, kuna kocha wa zamani wa Chelsea Andre Villa Boas na kocha wa Everton David Moyes… acha tusubiri tuone matokeo.


Bmw M6 2012
.
.
.
.
.
.


 
.
Serikali imetolea ufafanuzi ishu ya mkwanja ambao ni shilingi bilioni 3.5 ulioidhinishwa na wizara ya mambo ya nje yna ushirikiano wa kimataifa pamoja na utumishi wa umma kwa ajili ya safari ya Rais Jakaya Kikwete kuelekea nje ya nchi, pesa ambazo zilidaiwa kupotea kwenye mazingira ya kutatanisha  March mwaka huu.
Waziri wa wizara hiyo Bernard Membe baada ya kukutana na washika kalamu amesema fedha zote zimerejeshwa wizarani na kwamba tayari wizara imeunda kamati kuchunguza utaratibu uliotumika kuidhinisha fedha hizo, na kuongeza kwamba wakati wa uidhinishwa wa hizo fedha viongozi wote wa ngazi za juu wa wizara pamoja na muhasibu mkuu hawakuwepo.
Amesema “hizi fedha zote ziliingia kwenye account ya wizara na nyingine zikaletwa wizarani lakini hata senti moja haikuchukuliwa, tuliziona na zikahesabiwa na zilizofika hapa wizarani kwa nia ya safari zilirejeshwa benki kwa hiyo hayupo alieiba, tusimuhukumu mtu ambae hajaiba bado”
Kuhusu ishu yake kwamba amekitabiria chama cha CHADEMA ushindi katika uchaguzi mkuu ujao, Membe amesema  “ni kitu ambacho kiliwekwa makusudi ili kunifitinisha na Chadema na Wanaccm wenzangu nionekana wa ovyo tu nisikaribishe karibishe watu, hamna nitaendelea kukaribisha watu nyumbani kwangu… vijana wa Chadema walikuja kwa heshima zote nyumbani kwangu bahati nzuri walikuja wakati wa mlo wa mchana kama waliotea nikawakaribisha nilikua na marafiki zangu, walifurahi vizuri kweli”


.
Msichana wa miaka 16 nchini Kenya amefanya kituko baada ya kukosea na kupika bangi kama mboga kwa ajili ya chakula cha familia jioni huko Kiarimui kwenye wilaya ya Embu..
Standard Media wamesema baba mzazi wa huyo binti ambae ni mwalimu wa sekondari ana shamba nyumbani ambalo lina mboga mbalimbali ambazo huwa zinanawiri wakati wote, kiangazi na vuli.
Jioni hiyo mama wa huyo binti alimuagiza mwanae ambae amerudi nyumbani kwa likizo kwenye kupika ugali na mboga za majani, sasa mtoto alipokwenda shambani kuchukua mboga hakuweza kutofautisha bangi na mchicha.
.
Sasa noma ikawa kwenye msosi baada ya kuiva ambapo mtoto wa mwisho wa hiyo familia ambae ni wa kiume alianza kucheka kucheka ovyo na ndio alikua wa kwanza wa kupakua msosi mezani, alipomaliza kupeleka matonge mawili akasikia usingizi na kuzimika hapohapo, wengine pia walipakua msosi na kweli na wao wakaanza kucheka cheka ovyo.
Kingine cha ajabu wakati wako mezani kuna mjusi alipita ukutani alafu wote wakaanza kucheka na kutoa machozi baada ya kumuona, stori ilibadilika baada ya baba mwenye nyumba kuanza kumfokea mkewe huku akisema anawapa watoto kazi ambazo sio saizi yao.
Alipoinua mkono kumpiga mkewe na yeye kicheko kikamzidi ambapo kwa mujibu wa huyo mpishi kisa kizima kiliana kuwa kama movie na ikabidi waombe msaada kwa majirani ili kuelewa kilichotokea.
Baadhi ya majirani walifikiri kwamba huenda kuna majini yameipata hiyo familia ila wengine wakasisitiza hao watu wapelekwe kwenye kituo cha afya ambapo baada ya kupimwa damu zao zilikutwa zimejaa sumu ya dawa za kulevya, walitibiwa na kurudi nyumbani ila baba mwenye nyumba anakabiliwa na mashitaka ya kulima bangi shambani kwake.

Monday, June 18, 2012

HAPPY BIRTHDAY LADY JAY DEE











Na Waandishi Wetu
MSANII wa filamu Bongo aliyekuwa ameenda kupata matibabu katika Hospitali ya Saifee iliyopo jijini Mumbai, India, Sadick Juma Kilowoko ‘Sajuki’ amepata nafuu na kwa sasa anaendelea na dozi ili aweze kupona kabisa.
Akizungumza na Risasi Jumatano juzi nyumbani kwao Tabata jijini Dar, msanii huyo alisema sasa hivi afya yake imeimarika tofauti na alivyokuwa awali hivyo anawashukuru wote waliomsaidia na kwamba yeye hana cha kuwalipa ila Mungu atawalipa.
“Nina kila sababu ya kumshukuru Mungu kwani hali yangu inaendelea vizuri, kinachonisumbua ni ukali wa hizi dawa tu kwani kuna wakati mwingine nakosa nguvu lakini madaktari waliniambia nizitumie mpaka zitakapoisha,” alisema Sajuki na kuongeza:
“Pia niwashukuru Watanzania kwa michango yao, hakika wameonesha ubinadamu wa hali ya juu kwangu lakini nikanushe taarifa za kwamba nimerejea kama nilivyokwenda, kwa aliyeniona wakati naondoka atakubaliana na mimi kuwa afya yangu imetengemaa kwa kiasi flani.”
Mbali na shukrani kwa Watanzania, Sajuki aliwashukuru pia madaktari wa hospitali ya Saifee kwa uangalizi waliompatia ikiwemo kumpa chakula kizuri kilichokuwa kikihitajika kutokana na dawa anazotumia.
“Nawashukuru sana wale madaktari kwani wamenitibu chini ya uangalizi mzuri kiasi cha kunifanya nipate nafuu hii,” alisema.
Sajuki alianza kusumbuliwa na uvimbe mwaka jana ulioanzia mkononi kisha ndani ya mwili kwenye ini na baadae ikagundulika kuwa, siyo kwenye ini tu bali umesambaa hadi sehemu nyingine za tumboni.
Risasi Jumatano linamuombea kwa Mungu Sajuki apone kabisa, apate nguvu za kumuwezesha kurejea katika ulingo wa filamu ili aendelee kutuelimisha na kutuburudisha tunapokuwa tumejipumzisha majumbani mwetu.
Imeandikwa na Musa Mateja, Imelda Mtema na George Kayala.

Sunday, June 17, 2012

Kula aina mbalimbali za matunda kuna faida zaidi kiafya



Uchunguzi mpya umeonyesha kwamba watu wanaweza kukabiliana kirahisi na magonjwa mbalimbali kwa kula matunda ya aina mbalimbali na mboga mboga badala ya kuongeza idadi ya matunda na mboga mboga hizo. Kwa mujibu wa uchunguzi huo uliotolewa katika Kongamano la Majaribio ya Kibiolojia huko Anahein California, baadhi ya matunda na mboga mboga yana faida kubwa ya lishe kuliko mengineyo. Uchunguzi huo umeeleza kwamba,ingawa karoti inaaminiwa kuwa ni chanzo kikubwa cha beta-carotene lakini kula viazi vitamu badala ya karoti kunaweza kuupatia mwili beta-carotene mara dufu kuliko karoti. Papai nalo lina beta-cryptoxanthin mara 15 zaidi ya machungwa. Halikadhalika mboga aina ya Kale huupatia mwili mada ya lutein/zeaxanthin mara tatu zaidi ya spinachi. Pia imeelezwa kuwa stroberi na rasberi zina ellagic asid mara tatu zaidi huku kikombe kimoja cha maji yanayotokana na mmea uotao majini wa watercress ikiwa na mada ya isothiocyanate sawa na inayopatikana katika vijiko vine vya chai vya haradali au mustard. Bi. Keith Rabdolph aliyeongeza uchunguzi huo anashauri kwamba, watu wajitahidi kujua umuhimu wa vyakula wanavyokula na kujua pia ubora na faida za matunda na mboga mboga wanazokula kwa afya ya miili yao.


Kukosa usingizi kunasababisha vifo vya mapema


Imetahadharishwa kwamba kulala usingizi wa chini ya masaa 6 kila usiku kunaweza kusababisha mtu apatwe na kifo cha mapema. Watafiti wamesema kuwa watu ambao kwa kawaida huwa wanalala masaa hayo machache wengi wao hupatwa na vifo vya mapema kwa asilimia 12 zaidi ya wale wanaolala kawaida kwa masaa 8. Vifo ambavyo hutokea katika umri wa baada ya miaka 25. Pia imeonyeshwa kwamba kulala zaidi ya masaa 9 pia kunapelekea vifo vya mapema ingawa kulala huko kunaweza kukawa na uhusiano na matatizo ya kiafya. Utafiti huo umetolewa kwa kuchunguzwa uhusiano uliopo kati ya kifo na usingizi kwa kutegemea chunguzi 16 zilizofanywa kwa kuwahusisha watu milioni 1 na nusu katika nchi za Uingereza, Marekani , Ulaya na Mashariki mwa Asia.
Profesa Francesco Cappiccio aliyeongeza utafiti huo wa chuo kikuu cha Warwick cha Uingereza anasema jamii za hivi sasa zilizoendelea zimekuwa taratibu zikipunguza muda wa kulala, na tatizo hili linawapata sana watu wanaofanya kazi masaa mengi. Amesema suala hili linaonyesha kwamba hayo yote yanatokana na mashinikizo ya kimaisha yanayowapelekea watu wafanye kazi masaa mengi na kuchukua shift nyingi za kazi. Amesema kwamba, kuporomoka kwa afya kunaambatana na kulala masaa mengi zaidi. Wataalamu wanasema kuwa, watu wanapaswa kufahamu kwa nini hasa usingizi ni suala muhimu sana kwa afya nzuri. Usingizi ni kama karatasi ya litmus inayoonyesha afya na hali ya mwili na akili ya mtu kwani usingizi unaathiriwa na magonjwa na hali mbalimbali ikiwemo msongamano wa mawazo au depression, anasema mtaalamu huyo. Inashauriwa kuwa tusilale masaa machache wala mengi bali tulala kwa masaa ya wastani ambayo ni masaa 8.



Kweli lishe bora inaongeza umri…. Afa akiwa na miaka 114!


Mwanamke wa Kijapan aliyevunja rikodi ya Dunia ya Guinness kwa kuwa mtu mzee zaidi duniani amefariki dunia siku kadhaa zilizopita, akiwa na umri wa miaka 114 na siku 357. Mwanamke huyo aitwaye Kama Chinen alikuwa akiishi katika kisiwa cha Okinawa na alifariki dunia Mei 2, ambapo aliishi na kushuhudia karne tatu!. Inasemekana kuwa bibi huyo aliishi muda mrefu kwa kuwa lishe yake ilikuwa chai ya kijani, supu ya miso, mboga mboga, wali na samaki freshi. Bi. Chinen sio makazi pekee wa eneo hilo la Japan aliyeishi muda mrefu, kwani ripoti zinasema kuwa watu wengi wanaoishi eneo hilo huishi maisha marefu na ni kutokana na lishe yao. Japan ndio nchi inayoongoza kwa kuwa na kiwango kirefu zaidi cha maisha ya watu (Highest Life Expactancy) huku Okinawa ukiwa mji ulio na watu wengi wenye umri mrefu, suala ambalo linatokana na lishe bora na hali ya hewa ya kisiwa hicho.
Kwa mujibu wa utafiti, mji wa Okinawa una kiasi kidogo sana cha watu wenye magonjwa ya kensa, na hiyo inatokana na watu kula vyakula vyenye mafuta kidogo, kalori chache, ufumwele kwa wingi na mboga mboga na matunda kwa kiasi kikubwa. Pia suala lingine ni kujishughulisha kwao na wala sio kukaa tu


Kula zabibu usipatwe na ugonjwa wa moyo


Wadau msichoke na mimi kuzungumzia ugonjwa wa moyo, au nisiseme mimi, bali niseme wataalamu ambao kila siku wamekuwa wakifanya majaribio na kutuelewesha vyakula au njia zinazotuepusha na ugonjwa huu. Hii ni kwa sababu ugonjwa wa moyo kweli ni tishio duniani kote. Ni wiki iliyopita tu mfanyakazi mwenzangu ambaye nilikuwa naye kazini hadi nyakati za mwisho za kazi, siku ya pili nakuja kazini naambiwa kafariki dunia kwa mshituko wa moyo. Masikini baba wa watu!!, huku akiwa anayetegemewa na familia, akiacha mke na mtoto ameondoka kama utani tena kwa kufumba na kufumbua. Baada ya kutoka kazini alikaa juu ya kochi na kujiegemeza akisubiri atengewe msosi, lakini hapo hapo aliaga dunia. Msosi ulipotengwa na mkewe kumuamsha ale akidhani labda amepitiwa na usingizi, aliona haamki tena, na ndipo walipomkimbiza hospitalini. Huko waliambiwa ameshakufa zamaaani kutokana na mshituko wa moyo!.
Sasa hali ni hii, na hivi karibuni uchunguzi mpya umeonyesha kwamba kula zabibu au vyakula vyenye zabibu ndani yake kunapunguza shinikizo la damu, husaidia moyo kufanya kazi zake vyema na kupunguza hatari ya kupatwa na ugonjwa wa moyo.
Kwa mujibu wa uchunguzi huo uliotolewa kenye mkutano wa Majaribio ya Bayolojia huko California, zabibi zina uwezo wa kupunguza shinikio la damu, husaidia mwili uweze kuvumilia sukari (glucose tolorance) na kupunguza kiwango cha mafuta aina ya triglycerides mwilini ambayo ni chanzo cha matatizo ya moyo.

Wataalamu wanasema zabibu pia zinaweza kupunguza uvimbe, uharibivu unaotokana na free radicals zinazozalishwa mwilini na shinikizo la moyo.
Kwa ujumla zabibi zinazuia hali inayoitwa Metabolic Syndrome suala ambalo linatokana na mada za phytochemicals zilizoko kwenye matunda hayo.
Metabolic Syndrome ni mchanganyiko wa matatizo ya kitiba ambayo yanaongeza uwezekano wa kupatwa na maradhi ya mishipa ya damu pamoja na kisukari.
Hivyo wataalamu wanatushauri tule zabibi au kuongeza zabibu katika vyakula wanavyokula kila siku, ili tujikinge na ugonjwa wa Metabolic Syndrome, ugonjwa wa moyo na kisukari aina ya pili.
Haya shime tule zabibu kwa ajili ya afya zetu!.


Kuchoka wakati wa ujauzito na namna ya kujiepusha

Wapenzi wadau natumaini hamjambo! kumekuwa na baadhi ya wadau wanaoniandikia na kuomba ushauri mbalimbali kutokana na matatizo waliyonayo. Nawashukuru sana kwa kuwa wanafuatilia yale yanayojiri katika blogi hii na kupata ingawa machache kuhusiana na afya zetu. Pia nawashukuru kwa kuniwezesha nami kuzungumzia mada mbalimbali kutokana na maswali yenu munayoyauliza. Kwa wale wenye maswali na matatizo mbalimbali tafadhali sana niandikieni kwa kupitia email yangu ambayo ni sthugs4j@gmail.com. Kwani wale wanaoandika maswali yao katika sehemu ya maoni, baadhi ya wakati huwa siyaoni katika muda unaotakiwa na hivyo hunifanya nichelewe kuwajibu. Wote mnashukuriwa. Leo tutazungumzia suala la kujihisi uchovu wakati wa ujauzito ambalo limeulizwa na mmoja wa wadau wanaofuatilia kwa karibu kona ya afya nami nalijibu swali lake kama ifuatavyo.

Wanawake wengi kwa kawaida huwa wanahisi uchovu wakati wa ujauzito. Uchovu, kulegea mwili na kuishiwa na nguvu ni jambo la kawaida katika kipindi hicho. Hii ni kwa sababu mwili katika kipindi hiki unatumia nguvu za kiada ili kuunda kiumbe kipya. Pia wakati huu mwili hutengeneza damu kwa wingi zaidi ili kufikisha chembechembe za chakula kwa mtoto, suala ambalo huufanya mwili ufanye kazi ya ziada na hata viungo vingine muhimu kama vile moyo na vinginevyo. Uzito wa mtoto nao unaoongezeka katika mwili wa mama mjamzito siku baada ya siku, ni sababu nyingine inayomfanya mama mjamzito ajihisi kuchoka. Kuchoka au kiushiwa na nguvu ni tatizo la kawaida hasa katika miezi mitatu ya mwanzo ya mimba. Katika miezi hiyo ya mwanzo ya mimba tatizo hilo husababishwa na mabadiliko ya homoni za mimba mwilini hasa progestrogen na wakati mwingine hali hiyo huongezwa na kichefuchefu na kutapika. Hali hiyo ya mchoko inatarajiwa kuisha inapoingia miezi mitatu ya pili ya mimba. Lakini pia kuna wengine ambao hali hiyo ya kuchoka huendelea nayo hadi wakati wa kujifungua. Kushindwa kulala vizuri kutokana na kwenda mara kwa mara msalani, au kukosa uzingizi kutokana na ongezeko la ukubwa wa tumbo mwishoni mwa ujauzito, ni miongoni mwa masuala ambayo humfanya mama mjazito ajisikie mchovu na akose nguvu siku nzima.
Vilevile mabadiliko ya kifizikia na kisaikolojia ya wakati wa ujauzito humfanya mama mjamzito awe na morali ya chini na kuhisi uchovu wa kimwili na hata kiakili. Sababu nyinginezo zinaweza kutokana na kazi mbalimbali anazofanya mama huyo au pia ukosefu wa lishe inayofaa na ya kutosha kwa ajili ya mwili wake, ambao unahitajia nguvu ya ziada hasa kwa ajili ya uumbaji wa ukamilifu wa mtoto aliye tumboni.
La muhimu analoshauriwa mama mjamzito ni kutoogopa na kutotishwa na hali hiyo, kwani inatokana na baadhi ya mabadiliko yanayotokea katika mwili wake. La muhimu ni mama mjamzito kufuata ushauri unaotakiwa ili kukabilina na hali hiyo.
Zifuatazo ni njia za kukabiliana na uchovu wakati wa ujauzito.
• Kwanza kabisa mama mjamzito anatakiwa ale vyema. Mama mjamzito anatakiwa ale chakula bora na kamili, chenye kalori 300 au 500 za ziada ikilinganishwa na mtu asiye mjamzito kwa siku. Lakini awe mwangalifu na ni bora akigawe chakula chake katika sehemu ndogo ndogo 5 au 6 (suala hili tumelizunguzia kwa undani katika makala iliyopita ya kiungulia wakati wa ujauzito, tafadhali pitia makala hizo). Anaweza akawa akibeba matunda na mboga mboga kama asusa (snacks) kwa ajili ya kula kila anapohisi njaa popote pale awapo. Lakini ni bora ajiepushe na vyakula vyenye sukari nyingi na caffeine, kwani vyakula hivyo huyeyuka haraka mwilini na kumfanya ahisi njaa mapema.
• Mama mjamzito ahakikishe kuwa hana upungufu wa damu. Na kama anao basi atumie dawa za kuongeza damu zinazotolewa na madaktari, au ale vyakula vinavyoongeza damu. Hii ni kwa sababu ukosefu wa madini ya chuma mwilini unaosababisha ukosefu wa damu, ni miongoni mwa sababu zinazomfanya mama mjamzito ahisi kuchoka. Mtu mwenye ukosefu wa damu (Anemia) huhisi kubanwa na pumzi, ongezeko la mapigo ya moyo, udhaifu, kupauka na kizunguzungu. Onana na daktari iwapo una dalili kama hizo.



• Mama wajawazito wanashauri kujipumzisha nyakati za mchana. Ni bora mama mjamzito apumzike kwa kadri anavyoweza wakati wa mchana, baada ya chakula cha mchana au hata kabla ya nyakati za magharibi. Ikiwa unafanya kazi, basi pumzika mara kwa mara japo kwa muda mfupi ili kufanya mwili upate nguvu.
• Mama wajawazito wanashauriwa kujitahidi kulala mapema, hasa kama ikiwa inakubidi uamke mara kadhaa usiku kutokana na sababu mbalimbali, kama vile kwenda msalani, kula au kutokana na maumivu.
• Kufanya mzoeni husaidia kupunguza uchovu na kuna faida kemkem wakati wa ujauzito. Kahusiana na suala hilo soma makala zilizotangulia.
• Mama mjamzito anatakiwa anywe maji ya kutosha. Ukosefu wa maji mwilini huchangia kumfanya mama mjamzito ahisi uchovu.
• Usifanye kazi nyingi kutwa nzima, na kama inawezekana ni bora usaidiwe kazi hizo hasa za nyumbani na watu wengine katika familia kama vile watoto, mume ndugu, jamaa na marafiki.
• Usikilize mwili wako. Pale unaposikia njaa basi kula na pale unapojisikia uchovu jitahidi upumzike.
• Pata ushauri wa daktari iwapo unahisi uchovu wa kupindukia au unachoka kila mara, ili uwe na uhakika kuwa hakuna tatizo au hatari inayoweza kuhatarisha maisha yako na ya mtoto.


Kupewa watoto sukari kabla ya chanjo kunapunguza maumivu


Watafiti wa Canada wamesema kuwa, kuwapa watoto sukari kabla ya kupewa chanjo kunapunguza maumivu. Watafiti wa Chuo Kikuu cha Toronto wamesema kwamba watoto wachanga wakipewa matone machache ya maji ya sukari, kabla ya chanjo hawatolia au watapunguza kulia. Hayo yamesemwa baada ya watoto 1,000 wachanga kupewa maji ya glukosi kabla ya kupigwa sindano na kupunguza kulia kwa asilimia 20. Utafiti huo umechapishwa katika jarida la Mafanikio ya Magonjwa ya watoto na umetokana na matokeo ya majaribio 14 yaliyofanywa kuhusiana na suala hilo. DaktaArme Ohlsson aliyeongoza timu ya utafiti huo amesema kwamba umefanywa kwa watoto wasiozidi mwaka mmoja. Pia watatifi hao wamesema kwamba, matone machache tu au nusu kijiko cha maji ya glukosi au sackrosi pia hupunguza muda wa mtoto kulia. Pia wamewashauri maafisa wa afya wawape watoto sakrosi na glukosi kabla ya kuwapatia chanjo. Wamesema kwa kuwa vyakula vitamu vina uwezo wa kupunguza maumivu ndio sababu watoto wanapopewa glukosi kabla ya chanzo huwa hawalii.


DAWA ZA KIUNGULIA ZINASABABISHA MPASUKO WA MIFUPA



Taarifa mpya zinasema kwamba, maafisa wa afya wametahadharisha juu ya kutumiwa kwa muda mrefu dozi kubwa ya dawa za kuondoa kiungulia, (heartburn) na kusisitiza kwamba zinasababisha mifupa kupasuka. Dawa hizo ni zile zinazojulakana kama Proton Pumping Inhibitors (PPI) zinazozuia kiungulia na ambazo hutumiwa kudhibiti kiwango cha asidi katika tumbo na pia kutibu ugonjwa wa GERD au gastroesophageal reflux disease. Taarifa hizo zilizotolewa na Kitengo cha Kusimamia Vyakula na Dawa cha Marekani (FDA) zinasema kwamba, dawa hizo za kingulia huongeza uwezekano wa kupasuka mifupa ya nyonga (hip), mikono na ute wa mgongo kwa watu wazima, hasa iwapo dawa hizo zitatumiwa kwa mwaka mmoja au zaidi, au kwa dozi kubwa.
Joyce Korvick Mkurugenzi wa masuala ya usalama wa kitengo cha FDA anasema kwamba, kwa kuwa dawa hizo zinatumiwa sana na watu wengi, ni muhimu kwa watu wote kufahamu madhara yanayoweza kusababishwa na dawa hizo. Maafisa hao pia wamewataka madaktari kuwaandikia tu dawa hizo wagonjwa ambao hali zao ni mbaya mno, na kusisitiza kuwa faida ya dawa hizo pale zinapotumiwa mara chache ni zaidi ya hatari inayozisababisha.
Huko nyuma pia wataalamu walisema kwamba, dawa hizo za kutibu kiungulia zinahusiana na ongezeko la hatari ya maambukizo ya bacteria aina ya C. difficile anayesababisha ugonjwa wa kuharisha.
Dawa hizo ni kama zile za Emsomeprazole, Dexlansoprazole, Lansoprazole, Emprazole/Sodium Bicarbonate, Pantoprazole, Rabeprazole na Rabeprazole.
Ndugu mdau kama wewe ni miongoni mwa wanaotumia dawa hizo, basi jihadhari kabla ya hatari!